Wabunge wa UKAWA, Bakini Bungeni Mlisaidie Taifa

Nawaomba kwa ujumla wenu. Najua hamuivi na Naibu Spika kwa mnavyomlalamikia. Najua kuwa mmeshatangaza kutoka kila Naibu Spika anapoliongoza Bunge na mmekuwa mkitoka kweli. Najua mna malalamiko yenye mashiko. Najua mnalilia ulinzi na ustawi wa demokrasia ndani na nje ya Bunge.

Kesho,mjadala wa Bajeti utaanza. Naamini,wakosoaji ndiyo wafuatiliaji na wasomaji. Wasomaji wa nyaraka kwa haraka na baraka Bungeni ni Wabunge wa Upinzani. Ni Wabunge wa UKAWA. Wabunge wa CCM hupumbazwa na uchama na wingi wao.

Msipokuwepo kesho na kuendelea,Wabunge wa CCM hawataijadili Bajeti. Wataisifu;kuisifu Serikali; kumsifu Rais na Naibu Spika na kuiunga mkono bajeti kwa asilimia mia. Bajeti itakosa kuchambuliwa na kukosolewa. Bajeti ni moyo wa nchi. Isipowekwa sawa,wote tutaumia. 

Tafadhalini,Wabunge wa UKAWA bakini Bungeni muifinyange bajeti ya nchi. Fanyeni hivyo kwa kulisaidia Taifa. Msijali yatakayosemwa kuhusu kubaki kwenu Bungeni!

Mzee Tupatupa-Kilaza wa Lumumba,Dar es Salaam