Sumaye Ampa Makavu Magufuli......Lowassa Aahidi Kudhibiti Rushwa Ndani ya Siku 100

Jana  ilikuwa ni Septemba 26  ambapo  UKAWA waliendelea  na  mikutano  yao  ya  kampeni  za kuomba  ridhaa  ya kuchaguliwa na  wananchi .Jana  ilikuwa  ni  zamu  ya  wakazi wa Wilaya ya Hai ambapo  Waziri  Mkuu  wa  zamani, Fredrik Sumaye aliendelea na kazi ya kupangua mashambulizi ya CCM.


Sumaye aliitumia siku ya jana kumjibu Dk Magufuli aliyesema kuwa utafiti uliofanywa na Twaweza unaoonyesha anaongoza kwa asilimia 65, umempunja ushindi aliostahili.

Sumaye alisema Dk Magufuli hawezi kupata hata asilimia 40 ya kura na ndiyo maana amekuwa akitofautiana na mwenyekiti wake Rais Jakaya Kikwete.

Akizungumza katika mkutano huo wa kampeni uliofanyika Rundugai, Jimbo la Hai, Sumaye alisema Dk Magufuli amekuwa akikisahau hata chama chake na kuwataka wananchi wachague Tanzania ya Magufuli, huku akiomba wananchi wasichome godoro lote lenye kunguni badala yake waue kunguni waliopo kwenye godoro hilo.

“Haiwezekani mkalalia kitanda chenye kunguni si ndiyo,” alihoji Sumaye na kuitikiwa na wananchi “ndiyoooooo”.

“Amesahau hata kusema chagua CCM, anasema chagua Tanzania ya Magufuli,” alisema Sumaye na kuongeza kuwa Tanzania haiwezi kuwa ya Magufuli, bali ni ya Watanzania wote.

Sumaye alisema kuwa hali ya CCM ni mbaya na ndiyo maana wananchi wamechoka na hali zao ni mbaya.

“Wananchi wanataka mabadiliko, hakuna vita itakayotokea kama wanavyohubiri huo ni upuuzi mtupu,” alisema Sumaye.

Sumaye aliwaambia wananchi hao wa Rundugai kuwa nchi nyingi duniani zinapata mabadiliko kwa kubadilisha mfumo uliopo, hivyo wananchi wasiogope kwa kuwa CCM siyo mama yao, bali ni chama cha siasa.

Lowassa  Aahidi  Kudhibiti  Rushwa  Ndani  Ya  Siku 100
Wakati Sumaye akisema hayo ,mgombea urais kwa tiketi ya Chadema, Edward Lowassa  aliahidi kuhakikisha  anapambana na tatizo la rushwa ambalo limekuwa chanzo cha umasikini nchini.

"Siku 100 za serikali ya Chadema, tutaunda chombo kila wilaya ambacho kitakuwa ‘one stop centre’. Ukienda mjini kwa shughuli za kiserikali huduma zote zitakuwa sehemu moja, hii itaondoa urasimu na rushwa." Alisema  Lowassa.

Huku akionekana kujiamini kushinda katika chaguzi ujayo,Lowasa alisema atahakikisha anaongoza nchi kwa misingi ya haki na usawa huku akiahidi kutumia vema ilani ya ukawa kuhakikisha anapambana na rushwa.

Alisema kwa mara ya kwanza nchini Tanzania upinzani utachukua nchi  na  akasisitiza  kuwa  CCM  lazima  Ing'oke  mwaka  huu.

"CCM  lazima  ing'atuke  mwaka  huu, lakini  itang'atuka  kwa  kura  zenu, hivyo  nawaombeni  mtunze  sana  vichinjio  vyenu." Alisema  Lowassa  na  kuongeza;

“Wale wenzangu waliochukia mimi kuondoka CCM, sasa wameanza kukubali uamuzi wangu kwa kuwa CCM imeshindwa kuongoza nchi, haifai tena kuongoza kama Sumaye alivyosema.Hali ya wananchi ni mbaya sana."

Lowassa aliendelea kurudia ahadi zake za elimu bure kuanzia msingi hadi chuo kikuu, pia kuboresha maisha ya Watanzania waondokane na umaskini ambao kila siku amekuwa akisema anauchukia.

Katika mkutano huo, Lowassa alimsihi Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe kuendelea kuambatana naye kwenye kampeni ili aongeze nguvu kwenye timu yake.

Lowassa alisema Mbowe anaweza kufanya kampeni zake kwenye Jimbo la Hai na kuweka timu ambayo itamsaidia wakati atakapokuwa nje ya jimbo kumpigia kampeni mgombea urais.

Akizungumza kwenye mkutano huo, Mbowe aliiponda CCM akisema kwa sasa haijielewi kwa kuwa iko hoi.

Alisema katika uchaguzi huu hawatakubali kuibiwa kura huku akiwaomba askari wakae pembeni ya siasa na kulinda amani ili wanasiasa wacheze ngoma yao wenyewe.

“Askari wetu lindeni amani tuachieni CCM tucheze nao msipendelee upande wowote,” alisema Mbowe.